Swahili Tales/Kisa cha Hassibu karim ad dini na Sultani wa nyoka

From Wikisource
Jump to navigation Jump to search
Swahili Tales  (1870)  by Edward Steere
Kisa cha Hassibu karim ad dini na Sultani wa nyoka
English translation: The Story of Hasseebu Kareem ed Deen and the King of the Snakes
[ 332 ]

KISA CHA HASSIBU KARIM AD DINI NA SULTANI WA NYOKA.


Aliondokea mtu mganga sana, akakaa, hatta mwana mtoto asipate, siku nyingi. Naye tabibu mkuu, haina dawa moja ya ulimwenguni asiyoijua. Na elimu nyingi anayoijua. Akakaa, hatta alipokuwa mzee sana mkewe akachukua mimba, naye hana kitu zayidi ya vyuo vya dawa.

Akaugua yule mtu, akamwita mkewe, akamwambia, nipe chuo changu, akampa, akafunua akatezama ndani ya chuo, akamwambia, wewe una mimba, utazaa mtoto mwanamume, jina lake mwite Hassibu karim ad dini. Akafa babaye.

Akakaa manamke, hatta akazaa mtoto mwanamume, akamlea, hatta akawa mkubwa.

Yule mtoto akamwambia mamaye, jina langu nini? Akamwambia, ngoja, kesho tutafanya karamu, tutawaita watu, waje wale, nipate kukupa jina alionipa babayo.

Akakaa, assubui akafanya karamu kubwa, akawaita wanajimu, wakaja kula karamu, akawaambia, mtoto wenu leo nitampa jina alionipa babaye. Wakamwambia, mpe. [ 334 ]Akawaambia, jina lake, Hassibu karim ad dini. Wakamwambia, heri.

Akatiwa chuoni kusoma, alipokwisha soma, akatiwa kiwandani kushona nguo, asijue, akatiwa kufua fetha, asijue, killa kazi anayofundishiwa hajui. Mamaye akanena, bassi, kaa kitako, mwanangu. Akakaa kitako akila na kulala.

Akamwambia, baba alikuwa na kazi gani? Akamwambia, alikuwa tabibu mkuu sana. Akamwambia, viwapi vyuo vyake vya utabibu? Akamwambia, siku nyingi zimepita, katezame ndani, kana viko. Akaenda, akatezama, akaona vimeliwa na wadudu imesalia gombo moja, akatwaa, akasoma, akaona dawa zile zote.

Hatta siku hiyo wakaja jirani zake wakamwambia mamaye, utupe sisi huyu mtoto tukaende naye kuchanja kuni. Nao, wale watu wanne, kazi yao kuchanja kuni, wakija, wakiuza mjini. Nao hupakia kuni juu ya punda. Mamaye akawaambia, vema, kesho nitamnunulia punda, mfuatane nyote.

Assubui mamaye akamnunulia punda, wakaja wale watu, wakafuatana naye kazini. Wakaenda, wakapata kuni nyingi, wakaja nazo mjini kuza, wakagawanya fetha.

Na siku ya pili wakaenda tena, na siku ya tatu, na siku ya nne, na siku ya tano, na siku ya sita. Hatta siku ya sabaa, walipokwenda, kukatanda wingu, ikanya mvua, wakakimbia kujificha chini ya jabali.

Yule Hassibu amekaa mahala pekeyake. Akatwaa [ 336 ]jiwe, akagonga chini, akasikia panalia wazi. Akawaita wenziwe, akawaambia, hapa panalia wazi!

Wakamwambia, gonga, akagonga, wakasikia panalia wazi, wakamwambia, tuchimbe. Wakachimba, wakaona shimo kubwa, limekaa kana kisima, wakaangalia ndani mna asali, limejaa tele.

Wakaacha kuni, ikawa kuchukua asali, kulla siku. Na yule Hassibu ndiye, aliyeliona mbele ile shimo la asali. Wakamwambia, wewe ingia mmo ndani, ukiteka asali, ukatupe sisi, tukaende tukauze mjini, hatta tukiisha, tupate kugawanya fetha. Akanena, vema.

Ikawa kazi zao kulla siku miezi mitatu, wakapata mali mengi.

Hatta asali ilipokwisha, imesalia chini kabisa nako mbali, wakamwambia, ingia wewe ndani kule, ukwangue iliosalia chini, ukiisha, tutakupa kamba, ushike, tukupandishe juu. Yule akakubali, akakusanya, akawaambia, nipeni kamba. Wakamwambia, hapana kamba, ngoja kwanza, inakuja. Wakafanya shauri, wakasema, huyu na tumwache mumo humo ndani ya shimo, tugawanye sisi mali.

Akaondoka mmoja, akasema, mama yake, tutamwambiaje? Akaondoka mmoja, akajibu, akamwambia, tutamwambia, mtoto wako aliondoka, kwenda chooni, akakamatwa na simba, yeye na punda wake, nako ndani ya mwitu tusiweze kumtafuta sana, lakini tukasikia simba analia, tukajua aliyemkamata ni yeye simba.

Wakaenda zao mjini, wakamwambia mamaye. Mamaye akalia sana, akakaa matanga, hatta yakaisha. Wale wakagawanya fetha, wakasema, tumpelekee na mama ya rafiki yetu kidogo fetha, wakampelekea. Bassi kulla [ 338 ]siku, yule humpelekea mchele, yule humpelekea mafuta, humpelekea kitoweo, humpelekea nguo, kulla siku.

Bassi hapa, turejee aliko Hassibu.

Amekaa siku ya kwanza, siku ya pili, siku ya tatu, akajua wenziwe wamemtupa, akashukuru Muungu. Akatembea ndani ya shimo, shimo kubwa sana. Usiku hulala mlemle, assubui akiamka, hupata asali kidogo, akala. Hatta siku moja amekaa kitako anawaza, akaona nge akaanguka chini, mkubwa sana, akamwua.

Akakaa kitako, akafikiri, nge huyu anatoka wapi? Labuda pana tundu mahala, nitakwenda kutafuta. Akaenda, akaona tundu ndogo, aona mwangaza mbali sana, akachokora kwa kisu, ikawa tundu pana sana, akapita, anaona mbali weupe na mwangaza, akaenda. Hatta akifika, akaona kiwanja, ametokea mahala pakubwa sana.

Akaona njia, akafuata njia, akaenda, akaona nyumba kubwa ya mawe, akaona na viti vingi, na mlango wake wa thahabu, na kufuli yake ya thahabu, na ufunguo wake wa lulu, akatwaa, akafungua, ndani akaona sébule kubwa, na viti vingi, akaona kiti kimoja cha thahabu, kimenakishiwa kwa lulu na jawahir na fusfús, akaona na kitanda kimetandikwa sana vizuri, akaenda akalala.

Hatta marra hiyo asikia watu wanakuja wengi. Wakaja hatta nyumbani, wakaona mlango umefunguliwa, wakaingia ndani. Na yule anayekuja ndiye Sultani wa nyoka.

Asikari wake wakajaa uwanjani, yee na mawaziri wake wakapita ndani, wakaona ajabu, wakamwona mtu amelala [ 340 ]juu ya kitanda, na kile ndicho kitanda cha Sultani, anachokaa. Wakataka kumwua, akawaambia, mwacheni, msimwue, niwekeni kitini, waka'mweka juu ya kiti.

Akawaambia, mwamusheni polepole, wakamwamusha. Akaondoka, akakaa kitako, akaona nyoka wengi, wamemzunguka, akamwona yule mmoja mzuri sana, amevaa nguo za kifaume.

Akamwuliza, wewe nani? Akamwambia, mimi Sultani wa nyoka, na hii nyumba yangu; akamwuliza, na wewe nani? Akamwambia, mimi Hassibu karim ad dini. Watoka wapi? Akamwambia, sijui ninapotoka wala ninakokwenda. Akamwambia, starehe; akawaambia asikari wake, enendeni mkalete matunda yote mwituni, tumkerimu mgeni.

Wakaenda, wakaleta kulla tunda, waka'mwekea mbele sinia nzima, wakamwambia kula. Akala hatta akashiba, wakampa maji, akanywa. Bassi, akakaa kitako, wakazumgumza.

Yule Sultani wa nyoka akamwuliza Hassibu, nipe kisa chako, toka ulipotoka kwenu hatta leo. Akampa kisa chote kilichompata njiani hatta akafika pale.

Naye Hassibu karim ad dini akamwuliza Sultani wa nyoka, unipe kisa chako nawe, nipate kujua. Akamwambia kisa changu kikubwa sana.

Akamwambia, nalikaa zamani moja, tukaondoka hapa kwenda jabali Al Káf, kwenda kubadili hawa. Nikakaa hatta siku moja nikamwona mtu akija nikamwuliza, watoka wapi wee? Akaniambia, mimi natoka mjini kwetu, ninapotea katika barra. Nikamwambia, weye mtoto wa nani? Akaniambia, mimi jina langu Bolukia, na baba [ 342 ]yangu Sultani amekufa, nikaenda kufungua kasha, nikaona mkoba, nikaufungua, umetiwa kisanduku cha shaba, nikafungua, ndani umefungwa kwa joho, nikafunua joho, nikaona chuo, nikasoma mimi, nikaona sifa nyingi za mtume. Nikafanya shauko kumwona mtu huyu. Nikawauliza watu, wakaniambia, bado hajazaliwa. Nikasema, mimi nitapotea hatta nimwone. Nikaacha mji wangu na mali yangu, ni katika kupotea hatta sasa sijamwona mtu huyo.

Na mimi nikamwambia, utamwona wapi, hajazaliwa bado? Labuda ungalipata maji ya nyoka, ungaliweza kuishi, usife, hatta ukaonana naye, lakini sasa haifai, yako mbali maji ya nyoka.

Akaniambia, kua heri tena, nitapotea mimi. Nikamwambia, kua heri. Akaenda zake.

Hatta akafika Misri, akamwona mtu, akamwuliza, weye nani? Akamwambia, mimi Bolukia. Akamwuliza, na weye nani? Akamwambia, mimi jina langu Alfán. Akamwambia, unakwenda wapi? Akamwambia, mimi nimeacha mji wangu, na ufalme wangu, na mali yangu, namtafuta mtume.

Akamwambia, utamwona wapi weye, naye hajazaliwa bado? Lakini sasa tukamtafute Sultani wa nyoka, tukimpata huyu, atatupa dawa sisi tutakwenda hatta alipo nebii Sulimani; tutapata pete yake, tutawale sisi, na Majini yote yatakuwa chini yetu, tutakalo tutawaamru.

Akamwambia, mimi nimemwona Sultani wa nyoka katika jabali Al Káf. Akamwambia, twenende bass. Na yule Alfán moyoni mwake anataka pete ya nabii Sulimani apate kutawala, yee awe mfalme wa Majini na ndege. Yule Bolukia ataka kumwona mtume, ndio shauko yake.

[ 344 ]Alfán akamwambia Bolukia, sasa tufanye tundu ya kumtegea Sultani wa nyoka, akiisha ingia ndani ya tundu, tulifunge, tumchukue.

Akamwambia, haya. Akafanya tundu, akitia vikombe viwili, kimoja cha maziwa, kimoja cha mvinyo. Wakaenda hatta wakafika jabalini.

Nipo sijaondoka bado kwenda mjini kwangu. Wakaenda, wakaweka tundu ile, nikaingia ndani nikanywa mvinyo, nikanilevya, wakanifunga, wakanichukua.

Hatta nilipoamka, naona nimechukuliwa na watu, na yule Bolukia yuko ndiye alionichukua. Nikanena, waana Adamu si wema, wataka nini sasa? Wakaniambia, twataka dawa tupake miguuni mwetu, tukanyage bahari hatta tufike tunakotaka. Nikawaambia, twendeni.

Wakaenda nami hatta kisiwani, na kisiwa kile kina miti mingi. Na ile miti ikiniona hunena yote—mimi dawa ya fullani—mimi dawa ya fullani—mimi dawa ya kitwa—mimi dawa ya miguu—hatta ule mti ukasema, mimi, mtu akipaka miguuni hupita juu ya bahari.

Wakanena, ndio tutakao. Wakatwaa mwingi. Wakarudi, wakanipeleka hatta pale jabalini. Wakanifungua, wakaniachia. Wakaniambia, kua heri, nikawaambia, kuaherini.

Wakaenda zao, wakipata bahari hupaka miguuni, wakapita. Wakaenda vivyo hivyo hatta wakafika siku nyingi sana wakakaribia alipolala nabii Sulimani. Mahala karibu, Alfán akafanya madawa yake, wakaenenda.

[ 346 ]Naye nabii Sulimani anangojewa na Majini. Wakakaribia wale wawili, wakasikia mtu anasema. Na nabii Sulimani amelala na mkono ameuweka kifuani, na pete kidoleni. Yule mtu akamwambia, akamwita Bolukia, unakwenda wapi weye? Akamwambia, nimefuatana na Alfán, anakwenda twaa pete ile. Akamwambia, rudi weye, huyu atakufa.

Alfán akamwambia Bolukia, ningoje hapa weye. Akaenda yee, akikaribia kutaka kushika pete, akapigiwa ukelele, akarushwa hapa hatta kule. Akarudi, asikubali, akaenda marra ya pili akataka kuishika pete, akapuziwa, akateketea kamma jifu.

Na yule Bolukia anaona pia, akasikia mtu akimwambia, rudi, enda zako, huyu thalimu amekwisha kufa.

Akarudi Bolukia, akaja zake hatta njiani akaona bahari, akapaka dawa yake miguuni, akavuka, akaenda kisiwa kingine, hatta akaisha akapaka dawa tena akavuka. Ikawa ndio kazi yake siku nyingi sana, na miezi mingi, na miaka mingi inakwisha naye njiani.

Akaenda hatta siku moja akamtokea mtu, akamwona amekaa kitako, akampa salaam, naye akamjibu. Akamwuliza, weye nani? Akamwambia, mimi, jina langu, Jani Shah, weye nani? Akamwambia, mimi Bolukia, akamwuliza, wafanya nini hapa?

Pana makaburi mawili, na yule mtu amekaa katikati ya makaburi, hulia sana, kiisha akacheka, akashukuru Muungu. Akamwuliza, nipe kisa chako wewe. Akamwambia, kisa changu kikubwa, lakini nipe chako weye kwanza, umetoka wapi, unakwenda wapi?

[ 348 ]Akamwambia, miye ni mtoto wa Sultani, baba yangu amekufa, nimetawala mimi. Hatta siku moja nikafungua kasha la baba, nikaona mkoba, ndani na chuo, nikasoma chuo kile, nikaona sifa za mtume, nikafanya shauko sana ya kumwona, nikatoka mimi katika mji wangu, nikapotea katika mwitu kumtafuta mtu huyo. Na kulla mtu nimwonaye huniambia, hajazaliwa bado. Na hatta sasa ni katika mtafuta bado. Nikali nikienda katika barra.

Akamwambia, kaa kitako bassi, nikupe kisa changu toka mwanzo hatta sasa. Akamwambia, nipe, nimekwisha kaa kitako.

Akamwambia, mimi, jina langu Jani Shah, na baba yangu, jina lake Taighamusi, Sultani mkubwa. Naye kulla siku ikipata mwezi huenda mwituni kwenda kupiga nyama. Na mwanawe ni mimi tu mmoja, anipenda sana. Hatta siku hiyo nikamwambia, baba, tufuatane mwituni. Akaniambia, kaa kitako, usiende mahali. Nikalia sana mimi, baba yangu akaniambia, twende, usilie.

Tukaenda zetu mwituni, na watu wengi wanaokwenda. Hatta tulipofika mwituni tukala chakula, tukaisha, bassi kulla mtu tukaingia mwituni tupige nyama.

Na mimi na watumwa wangu, watu sabaa, tukaenda njia yetu ngine, hatta tukifika mwituni, tukaona paa mzuri mno tukamfukuza hatta baharini, tusimpate. Akaingia majini paa, tukatwaa mashua, tukaingia mimi na watumwa wangu watu wanne, wale watatu wakarudi kwa baba. Sisi tukamfukuza paa hatta tusiuone mji, tukamkamata paa, tukamchinja. Tulipokwisha mchinja, ukavuma upepo mwingi, tukapotea.

Wale watumwa, wale watatu, walipofika kwa baba yangu, akawauliza, yu wapi bwana wenu? Wakamwambia, [ 350 ]twalimfukuza paa, hatta tukafika pwani, yule paa akaingia baharini, wakaingia mashuani, yee bwana na watu wanne, wakamfukuza, sisi tukarudi.

Baba yangu akasema, mwanangu amekwisha potea. Akaenda zake mjini, akakaa matanga, akashukuru Muungu.

Sisi tukaangukia kisiwani. Pana ndege wengi. Tukatafuta matunda tukala, tukatafuta na maji tukanywa. Hatta usiku, tukapanda juu ya mti tukalala. Alfajiri tukaingia mashuani mwetu, tukapotea, tukafika kisiwa kingine cha pili, hapana mtu awaye yote. Tukashuka, tukala matunda mengi, hatta usiku tukapanda juu ya mti, tukalala, wakaja nyama mbwayi, wakacheza sana.

Hatta assubui tukakimbia, tukaenda kisiwa cha tatu, tukifika tukitafuta matunda, tukaona mtofaa umezaa sana. Tukitaka kuchuma, tukasikia mtu, akatukataza, akinena, msichume, mtofaa u wa mwenyewe mfalme, nimewekwa kuungojea. Hatta usiku, wakaja kima wengi, wakafurahi sana walipotuona sisi, wakatutafutia matunda wakaletea, tukaja, tukala, hatta tukashiba.

Wakasema, mtu huyu tumfanye Sultani wetu. Yule mmoja akanena, watakimbia assubui hawa. Wakasema, kaivunjeni mashua yao. Wakaenda, wakaivunja.

Hatta assubui tukiondoka kukimbia, tukaenenda pwani, mashua yetu imevunjwa. Bassi, tukarudi, tukakaa kitako wakatuletea chakula, tukala, na maji, tukanwa. Na wale kima wanatupenda sana sisi, hawatupendi kuondoka. Siku nyingi tukakaa.

Hatta siku moja tukaenda kutembea, tukaona nyumba [ 352 ]kubwa ya mawe, na mlango wakwe umeandikwa. Nikasoma mimi, ya kwamba, mtu anaokuja hapa kisiwani, hawa kima hawamwachi kumpenda mno mfanya ndio mfalme wao. Na atakapokwenda zake, hapati njia, lakini iko njia moja, imelekea kibula, hufuata njia hiyo, hutaona uwanja mkubwa, una simba na chui na nyoka, mtapigana nao, mkiwashinda, mtapata njia, mtakwenda mbele, mtaona uwanja mgine, una tungu wakubwa, kana mbwa, na meno yao kana mbwa, wakali sana, mtapigana nao, mkiwashinda, mtapata njia ya kupita.

Tukafanya mashauri, wale watumwa wangu wakaniambia, tuenende, tukapone ao tukafe, na sisi sote tuna selaha zetu.

Tukaenenda hatta tukafika uwanja wa kwanza, tukapigana, wakafa watumwa wangu wawili. Tukaenda zetu, tukapita, tukaenda wa pili, tukapigana, wakafa watumwa wangu wawili, nikapona mimi.

Nikapotea siku nyingi, hatta nikatokea mji. Nikakaa kitako pale mjini, nnatafuta kazi, sipati. Akatokea mtu, akaniambia, wataka kazi? Nikamwambia, nataka. Akaniambia, twende zetu, tukaenda kwake.

Akachinja ngamia, akatwaa ngozi ile, akaniambia, nitakutia ndani ya ngozi, wende juu ya jabali, ndege atakuchukua, ukifika atakufungua, usukume vito chini, ukiisha nitakushusha mimi.

Akanitia ngozi ile, akaja ndege, akanichukua akaniweka juu ya jabali, akataka kunila, nikaondoka, nikamfukuza ndege, akaruka. Nikasukuma vito chini vingi, nikamwambia, nishushe, bass! Asinijibu neno, akaenda zake.

[ 354 ]Nikasema, nimekufa mimi. Nikaenenda mwituni siku nyingi. Nikatokea nyumba moja, nikamwona mzee katika nyumba, akanipa chakula na maji, nikashukuru Muungu.

Nikakaa kitako pale, akanipenda kana mwanawe. Akanipa funguo zote za nyumba, akaniambia, fungua kulla utakapo, ela chumba hiki kimoja usifungue. Nikamwambia, vema, baba.

Nikakaa, akatoka yee kwenda kutembea, nikafungua mimi, nikaona bustani kubwa, na mto unapita. Marra wakaja ndege watatu, wakatua pale mtoni. Marra wakageuka watu, wakaoga mtoni, na wazuri mno wale watatu waanawake. Nikawatezama hatta walipokwisha kuoga, wakavaa nguo zao, wakaruka.

Nikarudi mimi, nikafunga mlango, nisiweze kula kitu. Hatta baba yangu akaja, akaniuliza, una nini? Nikamwambia, nimekwenda katika bustani, nimeona waanawake watatu, wamekuja kuoga, wamekwisha, wameruka, na yule mmoja nampenda mno, nataka kumwoa, kama sikumpata nitakufa.

Akaniambia, wale hawapatikani, wale watoto wa Sultani wa majini, na kwao mbali sana, mwendo miaka mitatu. Nikamwambia, sijui, sharti unipatie. Akaniambia, ngoja marra hii, watakapokuja kuoga, ujifiche, utwae nguo za yule umpendaye sana.

Nikaenda nikangoja, hatta walipokuja wakavua nguo zao, nikazitwaa, nikazificha. Na yule ndio mdogo wao, na jina lake Seyedati Shemsi. Walipotoka wakavaa nguo zao, wale nduguze, yee akatafuta zake, asizione. [ 356 ]Nikamwambia, ninazo mimi. Akaniambia, nipe mwenyewe, nataka kuenda zangu. Nikamwambia, mimi nakupenda sana, nataka kukuoa. Nataka kwenda kwa baba yangu. Nikamwambia, huendi.

Wakaruka wale nduguze, wakaenda zao, nikamchukua kwetu, yule baba yangu akanioza. Akaniambia, nguo hizi usimpe, zifiche sana, akizipata mwenyewe, ataruka kwenda zake kwao. Nikazichimbia chini, nikazitia.

Hatta siku hiyo nimetoka kwenda kutembea, akazifukua, akazivaa mwenyewe akaruka, akakaa juu ya dari, akamwambia mtumwa wake, bwana wako akija mwambia nimekwenda zangu kwetu, kama anipenda anifuate. Akaruka, akaenda zake.

Hatta nilipokuja, nikaambiwa, mkewo amekwenda zake kwao. Nikapotea nikimfuata miaka mingi.

Hatta nilipofika karibu na mji nikaona watu, wakaniuliza, weye nani? Nikawaambia, mimi Jani Shah. Mtoto wa nani? Nikawaambia, mtoto wa Taighamusi. Wakaniambia, weye ndiye uliye umeoa bibi yetu? Nikawauliza, nani bibi yenu? Wakaniambia, Seyedati Shemsi. Nikawaambia, miye. Moyo wangu ukafurahi sana.

Wakanichukua hatta mjini kwao. Akamwambia babaye, huyu ndio mume wangu aliyenioa. Nikapendwa sana, nikakaa siku nyingi.

Babaye akaniambia, mchukua mkewo, kama wataka kwenda kwenu. Tukapewa Majini, wakatuchukua kwa siku tatu. Tukafika, tukakaa mwaka.

Nikasema, twende, tuangalie baba yetu. Mke wangu akaniambia, twende. Hatta tukifika hapa, mke wangu [ 358 ]akaenda kuoga. Hatta akitoka, amekufa, nikamzika hapa. Wale Majini wakaenda kwa babaye kumwambia, mwanawo amekufa. Babaye akasema, kamwiteni Jani Shah, aje, aoe huyu mtoto mgine. Wakaja kuniambia. Nimesema, sitaki, nitachimba kaburi la pili, nikifa, niingie ndani. Ndio kisa changu.

Akakaa hatta akafa. Na yule Bolukia akaenda zake, akafa njiani.

Sultani wa nyoka akamwambia Hassibu, na wewe ukienda kwenu utanifanya vibaya. Akamwambia, sitakufanya vibaya, nipeleke kwetu. Akamwambia, miye najua, nikikupeleka kwenu, utarudi, uje, uniue. Akamwambia, sithubutu, nipe kiapo, niape. Akampa watu, wakampeleka kwao. Akamwambia, ukifika kwenu, usiende kuoga panapo watu wengi. Akamwambia, siendi. Wakampeleka kwao, hatta walipofika, wakarudi wale, wakamwambia, kua heri. Akaenda kwa mamaye, akafurahi sana mamaye.

Na mle mjini mwao, Sultani hawezi sana, na dawa yake sharuti apatikane Sultani wa nyoka, auawe, nyama yake itokoswe, ndio dawa.

Yule waziri akaweka watu katika hamami, akawaambia, akija mtu kuoga ana alama tumboni mkamateni.

Yule Hassibu akakaa siku tatu, akasahau maneno ya yule rafiki yake Sultani wa nyoka, akaenda kuoga.

Wale asikari wakamkamata, wakampeleka kwa waziri. Waziri akamwambia, utupeleke mahala alipokaa Sultani wa nyoka. Akamwambia, sipajui. Akawaambia, mfungeni. Akafungwa akapigwa sana, akapasukapasuka maongoni. Akawaambia, nifungueni, niwapeleke.

[ 360 ]Wakafuatana, wakaenda, hatta walipofika, Sultani wa nyoka akamwambia, sikukwambia, utakuja niua? Akamwambia, si mimi, na angalia maongoni mwangu. Akamwuliza, nani amekupiga hivi? Akamwambia, waziri. Akamwambia, bassi, sasa mimi nimekwisha kufa, lakini sharti unichukue wewe hatta kwenu. Akamchukua, na wale asikari wakarudi, na yule waziri yumo mlemle.

Akamwambia njiani rafiki yake, mimi nikifika nitauawa, na nyama yangu itapikwa, povu la kwanza, waziri atakwambia kunywa wewe, nawe usinywe, litie chupani, u'mwekee, la pili kunywa wewe, utakuwa tabibu mkubwa, la tatu ndio dawa la Sultani wenu. Na hili la kwanza akija akikuuliza, umekunywa wewe la kwanza? Mwambie, nimekunywa, na hili la pili lako weye. Waziri atapokea, akiisha kunywa, atakufa, utapumzika roho yako.

Wakaenda zao, hatta wakafika mjini, wakafanyiza vilevile kama alipomwagiza rafiki yake.

Yule waziri akanywa, akafa, na lile la pili akanywa yeye, na la tatu akamfanyia dawa la Sultani, akapona.

Akampenda sana Sultani, akawa tabibu mkubwa katika mji, akakaa raha kwa uzima hatta khatima.